Tanzania inaongeza kasi ya uwekezaji katika miundombinu ya nishati ili kuendeleza malengo yake ya uzalishaji wa viwandani na kujitokeza kama kitovu kipya cha viwanda cha Afrika Mashariki.
Umeme wa uhakika na wa bei nafuu unabaki kuwa kiini cha mkakati wa kiuchumi wa nchi. Kwa kulenga upanuzi na utofauti wa vyanzo vya nishati, Tanzania inajenga msingi wa uendelevu wa viwanda na ushindani wa muda mrefu.
“Miundombinu ya nishati mara nyingi ndiyo dhamira ya kwanza katika mnyororo wa viwanda kwa sababu ndiyo inayosukuma mambo mengine yote kusonga mbele,” anasema Elias Ngunangwa, Mkuu wa Idara ya Wateja wa Kampuni na Uwekezaji katika Benki ya Stanbic Tanzania. “Dhamira hiyo inapokaa sawa, inafungua mlango wa maendeleo katika uzalishaji na uundaji wa ajira.”
Sera ya kitaifa ya nishati iliyoanzishwa mwaka 2015 imeweka maendeleo ya miundombinu kuwa kiini cha mpango wa viwanda wa Tanzania. Umeme wa maji kwa sasa unachangia takriban asilimia 60 ya uzalishaji wa taifa, lakini utegemezi wa mvua umeonyesha umuhimu wa kuwa na mchanganyiko mpana zaidi wa nishati. Hali hii imeisukuma serikali kupanua miradi ya nishati mbadala na kutumia ipasavyo akiba ya gesi asilia ili kuhakikisha utulivu.
“Tanzania imebarikiwa kuwa na akiba kubwa ya gesi asilia, ikiwemo eneo la Songo Songo, jambo linaloimarisha nafasi yake kama kinara wa nishati katika ukanda huu,” anafafanua Ngunangwa. “Gesi inasaidia upatikanaji wa uhakika wa nishati kwa viwanda na inaunga mkono malengo ya nchi ya viwanda.”
Gesi asilia kwa sasa inaendesha zaidi ya viwanda 45 vikubwa jijini Dar es Salaam, na kuhakikisha upatikanaji endelevu wa nishati kwa sekta kama saruji, chuma, na nguo. Miradi hii haiboresha tu usalama wa nishati bali pia inaongeza ushindani wa Tanzania katika biashara ya kikanda.
Tanzania pia inaendeleza ushirikiano wa nishati wa kuvuka mipaka kama sehemu ya hifadhi ya umeme ya Afrika Mashariki. Nchi tayari inauza umeme wa ziada kwa mataifa jirani wakati wa upungufu, hatua inayoongeza uthabiti wa kikanda na ujumuishaji wa kiuchumi.
Kadri miundombinu ya nishati inavyopanuka, ufadhili bunifu unazidi kuwa muhimu. Benki ya Stanbic Tanzania inachukua nafasi ya juu kwa kubuni suluhisho za kifedha zinazolingana na mahitaji ya miradi mikubwa ya nishati na viwanda.
“Tunaenda zaidi ya mikopo ya kawaida,” anasema Ngunangwa. “Tunaunda suluhisho za kifedha zinazokidhi mahitaji maalum ya sekta ya nishati ya Tanzania na kuwaunga mkono wawekezaji kupitia programu za kujenga uwezo zinazowawezesha kuelewa soko vizuri.”
Mifumo mbadala ya ufadhili kama vile hati fungani za kijani (green bonds) na ubia kati ya sekta za umma na binafsi (PPP) zimepata kasi, na kuwezesha maendeleo ya haraka ya miradi ya usafirishaji na uzalishaji wa umeme. Kulingana na David Kafulila, Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Ubia kati ya Sekta ya Umma na Binafsi chini ya Wizara ya Fedha, PPP zinaiwezesha serikali kukusanya mtaji binafsi na utaalamu wa kiufundi huku zikpunguza utegemezi wa mikopo au kodi.
“Ubia huu unaharakisha utekelezaji wa miundombinu muhimu, jambo lililo la msingi kwa ukuaji wa viwanda,” anafafanua Kafulila.
Mtazamo wa Benki ya Stanbic unalenga kujenga uhusiano wa muda mrefu katika mnyororo mzima wa thamani, kuhakikisha ushirikiano endelevu katika sekta muhimu kwa ukuaji wa Tanzania.
“Tunajenga uhusiano kwa kuzielewa kampuni zetu, kukusanya maarifa, na kuyatafsiri maarifa hayo kuwa thamani,” anasema Ngunangwa.
Kupitia uwekezaji endelevu, utofauti wa vyanzo, na ushirikiano, Tanzania inaweka msingi imara wa mabadiliko ya viwanda. Kwa kuwa na nishati ya uhakika na ushirikiano wa kimkakati unaoendesha maendeleo, nchi inajipanga hatua kwa hatua kuwa kitovu cha uzalishaji na nishati kinachoongoza Afrika Mashariki.
0 Comments