...............................
Na Dotto Mwaibale, Dodoma
SAKATA la Mgonjwa
Ester John Furaha aliyedai kuzuiliwa katika Hospitali ya Benjamin Mkapa Jijini
Dodoma kwa kushindwa kulipa gharama ya matibabu licha ya kupewa rufaa kwenda
Taasisi ya Kansa ya Ocean Road jijini Dar es Salaam limefikia tamati baada ya
kuruhusiwa.
Akizungumza Machi
20, 2026 na mwandishi wa habari hii, Afisa Uhusiano katika Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH), Jeremia
Mwakyoma alisema tayari mgonjwa huyo ameruhusiwa kwenda kuendelea na matibabu yake Taasisi ya Kansa Ocean Road Jijini Dar es Salaam.
“Kuna rufaa za aina mbili ipo ya kawaida na nyingine anaposafirishwa inahitajika mgonjwa kuwekewa oksijeni ya kupumulia kama inavyohitajika kwa Ester lakini bila ya hivyo ataweza kupoteza maisha,” alisema Mwakyoma.
Mwakyoma
alisema kwa kawaida mgonjwa akipatiwa rufaa hata kama alikuwa na deni hawezi
kuzuiliwa atakwenda hospitali husika na suala la malipo ya deni lake yatafuata
baadae wakati akiendelea na matibabu.
Awali mdogo
wa mgonjwa huyo Celina Furaha alisema kuwa dada yake alizuiliwa kutoka hospitali
hapo mpaka alipe deni la Sh. 1,175,000
alizokuwa akidaiwa baada ya kupatiwa matibabu na kueleza kuwa rufaa hiyo alipewa Machi
18, 2026.
“Tumeruhusiwa leo Machi 20, 2026 kuondoka kuelekea Taasisi ya Kansa ya Ocean Road jijini Dar es Salaam kwa ajili ya matibabu tunashukuru sana na Mungu hawabariki ingawa nilitamani turudi nyumbani tukatafute hela za matibabu,” alisema Celina.
Celina alisema
wamekuwepo katika hospitali hiyo kwa zaidi ya miezi mitatu wakitokea Hosptali
ya Makiungu wilayani Ikungi mkoani Singida ambapo walibaini kuwa anasumbuliwa na
ugonjwa wa kansa na wamelipia matibabu yake zaidi ya Sh. Milioni 3.2 na
kuishiwa fedha huku wakiishi kwa msaada wa wasamaria wema.
Mwaka jana
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu wakati akihutubia katika uzinduzi wa kampeni
za Chama Cha Mapinduzi (CCM), Kawe jijini Dar es Salaam moja ya ahadi yake
ilikuwa ni kupiga marufuku kuzuia miili ya marehemu ambayo ilikuwa ikizuiliwa
kwa kushindwa kuilipia katika hospitali mbalimbali nchini.
Hata hivyo katika
hali ya kawaida kwa wagonjwa kama Ester inapaswa kuwekwa mwongozo wa wazi ili
kuondoa hali hiyo ya kuzuiliwa kufuatia kuwa na deni badala yake wapelekwe haraka
kuendelea kupatiwa matibabu jambo litakalosaidia kuokoa maisha yao kuliko kuzuiliwa wodini kama ilivyodaiwa kufanywa kwa
mgonjwa huyo.
Kwa ujumla hatua
ilichukuliwa na Hospitali ya Benjamin Mkapa (BMH) kumruhusu mgonjwa huyo kwenda
kuendelea kupata matibabu yake Taasisi ya Kansa ya Ocean jijini Dar es Salaam inapaswa
kupongezwa.
Taarifa hii imeandikwa na Dotto Mwaibale simu namba 0754362990.




0 Comments