Subscribe Us

WABUNGE MANYARA SIKIENI OMBI LA MPIGA KURA WENU

 

Mgonjwa Ester John Furaha
.........................

Na Dotto Mwaibale, Dodoma

WABUNGE wa Mkoa wa Manyara wakiongozwa na Naibu Spika wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Daniel Sillo, wananchi wa Manyara na Watanzania  kwa ujumla, mgonjwa Ester John Furaha ambaye anapitia wakati mgumu kutokana na ugonjwa wa kansa unaomsumbua anaomba msaada wenu.

Ester John Furaha anayesumbuliwa na kansa ya kichwa hali yake imetetereka licha ya kupata matibabu katika hospitali mbalimbali na anakabiliwa na madeni makubwa kutokana na fedha anazokopa kwa ajili ya matibabu.

Mapema wiki hii (Machi 18, 2026) baada ya kupewa rufaa ya kwenda kutibiwa Taasisi ya Kansa Ocean Road Jijini Dar es Salaam inadaiwa  alizuiliwa Hospitali ya Benjamin Mkapa Jijini Dodoma mpaka alipe Sh.1, 175, 000 alizokuwa akidaiwa baada ya kutibiwa.

Mgonjwa huyo Machi 20, 2026 aliruhusiwa kuondoka katika hospitali hiyo akiwa na mdogo wake Celina anaye muuguza baada ya habari yake kusambaa kwenye mitandao ya kijamii.

Akizungumza na mwandishi wa habari hii, Celina Furaha (27) alisema wao ni wakazi wa Kijiji cha Changanyika kilichopo Katesh wilayani Hanang’ Mkoa wa Manyara.

Celina alisema dada yake Ester mwenye watoto wanne alianza kuumwa mwaka juzi ambapo alikuwa akitibiwa Hospitali ya Tumaini iliyopo Hanang’ mkoani humo lakini pamoja na kupata matibabu hali yake iliendelea kuwa mbaya.

Alisema mume wake alipoona ameelemewa na madeni baada ya kukopa fedha kwa ajili ya matibabu yake alikimbia na mpaka sasa hajulikani alipo.

“Mume wake baada ya kuona amezidiwa na madeni aliondoka bila ya kuaga na hatujui halipo hivyo tunaangaika na mgonjwa huku tukikabiliwa na madeni makubwa ambayo sijui tutayalipaje,” alisema Celina.

Alisema baada ya hali yake kuzidi kuendelea kuwa mbaya alipewa rufaa ya kwenda Hospitali Teule ya Makiungu iliyopo Wilaya ya Ikungi mkoani Singida ambapo alitibiwa kwa wiki kadhaa na baada ya vipimo aligundulika kuwa na kansa kwenye kichwa.

Aliongeza kuwa baada ya hapo alipewa rufaa ya kwenda Hospitali ya Benjamin Mkapa lakini hata hivyo walilazimika kukaa katika hospitali ya Makiungu mpaka walipopata fedha Sh. Milioni moja waliyokopa ambayo iliwasaidia kuanza kupata matibabu hospitali ya Benjamin Mkapa jijini Dodoma.

Alisema tangu wawepo katika hospitali hiyo wametumia zaidi ya Sh. Milioni 3.2 ambazo wamezikopa kwa watu mbalimbali na wanadaiwa.

Aidha, Celina alisema hawana mtu wanayemtegemea zaidi ya kilimo cha mkono  kwani baba yao alifariki na mama yao ni mlemavu wa macho (haoni) na pia anasumbuliwa na ugonjwa wa kifafa.

“Tunapita katika wakati mgumu maisha yetu ni ya mateso tumekuwepo hapa hospitalini kwa zaidi ya miezi mitatu tukipatiwa msaada wa chakula na mambo mengine na wasamaria wema ambao wanafika kuwaona ndugu zao ambao ni wagonjwa,” alisema Celina huku akikata tamaa na kutamani warudi nyumbani kwao Katesh.

Mgonjwa Ester na mdogo wake anayemuuguza tayari wameondoka jana Machi 20, 2026 majira ya saa 9 mchana kuelekea Taasisi ya Kansa ya Ocean Road jijini Dar es Salaam huku wakiwa hawajui hatima yao watakapokuwepo kwenye jiji hilo kubwa ambapo watahitaji chakula, matibabu na mambo mengine ya kibinadamu.

Kupitia habari hii Celina anawaomba wabunge wa Mkoa wa Manyara wakiongozwa na Naibu Spika Daniel Sillo, viongozi na makundi mengine na Watanzania kwa ujumla waweze kuwasaidia katika wakati mgumu wanaopitia ikiwa pamoja na kulipa madeni wanayodaiwa.

Kwa mtu yeyote atakaye guswa kuwasaidia anaweza kuwasiliana na mwandishi wa habari hii kwa namba 0754362990, Mungu atawabariki.

Taarifa hii imeandaliwa na Dotto Mwaibale namba ya simu 0754362990.


Post a Comment

0 Comments